
RAIS William Ruto ameweka wazi tofauti kati ya viongozi wa upinzani ambao yuko tayari kufanya nao kazi huku akiweza kuwa hawezi kushirikiana kisiasa tena na Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.
Katika mahojiano na Taifa Dijitali katika Ikulu ya Nairobi, Rais Ruto alisema yuko tayari kushirikiana na viongozi kutoka pande zote za kisiasa, lakini akasema hawezi kufanya kazi na kiongozi anayechochea ukabila, anayetoa matamshi ya kugawanya Wakenya au kuwatusi raia wengine.
“Ninaamini katika demokrasia na hapa Kenya watu hufanya kazi na kila mtu. Hata hivyo, sitakuwa tayari kufanya kazi na kiongozi ambaye haamini katika umoja wa taifa.” akasema Rais Ruto.
Alisisitiza kuwa hawezi kushirikiana na mtu anayehusika na “ubaguzi wa kikabila” au kutumia maneno yanayolenga jamii nyingine. Pia alisema hana muda na viongozi wanaowatusi wanawake kwa kutumia lugha chafu.
Kauli hizo zinaonekana kueleza kwa nini uhusiano wake wa kisiasa na Bw Gachagua ulivunjika, licha ya wawili hao kuwa washirika wakuu katika ushindi wa Kenya Kwanza mnamo 2022.
Rais Ruto alitofautisha uhusiano wake na aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga marehemu, akimtaja kama “mtu wa kipekee”. Alisema walifanikiwa kugeuka kuwa wapinzani hadi washirika katika serikali ya mseto kwa sababu walikuwa na maono yanayofanana kuhusu mustakabali wa Kenya na walikubaliana kuzima ukabila.
Kwa hivyo, ujumbe wa Rais haukuwa kwamba hataki kufanya kazi na viongozi wa upinzani, bali kwamba ushirikiano huo lazima ujengwe kwa misingi ya umoja wa kitaifa, kuheshimu jamii zote, Katiba na kuweka maslahi ya nchi mbele ya siasa za kikabila.
Hapo ndipo Bw Gachagua anakuwa tofauti, kwa mtazamo wa Rais. Kiongozi wa DCP amejijenga kisiasa kupitia kujenga himaya yake Mlima Kenya na sasa ni mmoja wa viongozi wakuu wanaopinga serikali ya Rais Ruto.
Bw Gachagua, pamoja na viongozi wa upinzani akiwemo Kalonzo Musyoka wa Wiper, Dkt Fred Matiang’i wa Jubilee, Martha Karua wa PLP, Justin Muturi wa DP na Eugene Wamalwa wa DAP-Kenya, wameunda muungano wa kisiasa kwa lengo la kumng’oa Rais Ruto madarakani.
Mnamo 2022, Bw Gachagua alikuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto na alichangia pakubwa kumsaidia kupata uungwaji mkono wa Kenya Kwanza katika eneo la Mlima Kenya.
Hata hivyo, uhusiano wao ulizorota baada ya kuingia serikalini, hatimaye kusababisha Bw Gachagua kuondolewa katika wadhifa wa Naibu Rais kupitia bungeni mnamo Oktoba 2024.
Tangu aondoke serikalini, Bw Gachagua amejitokeza kama sauti kuu ya Mlima Kenya na mpinzani mkali wa Rais Ruto. Kauli zake zimekuwa zikilenga zaidi maslahi, malalamishi na ushawishi wa kisiasa wa eneo hilo.
Rais Ruto alisema aina hiyo ya siasa ndiyo hawezi kuikubali, akiwataja viongozi wanaowagawa Wakenya kuwa wasaliti na maadui na kutumia siasa za kikabila kuwadharau wengine.
Pia alitetea kuondolewa kwa Bw Gachagua kama naibu rais, akisema mchakato huo ulikuwa wa kikatiba na uliotekelezwa na wabunge.
“Kutimuliwa kwake kulikuwa zoezi la kikatiba lililofanywa na wabunge,” akasema Rais.
Mzozo kati ya wawili hao ulikuwa umejikita katika masuala ya uteuzi wa viongozi, ugavi wa rasilimali za serikali, nafasi ya Mlima Kenya serikalini na mwelekeo wa utawala.
Bw Gachagua alikuwa akiishutumu serikali kwa kupuuza Mlima Kenya, huku washirika wa Rais wakimpinga kwa kuendesha ajenda ya kieneo badala ya kuzingatia maslahi ya kitaifa.
Sasa, wawili hao wako pande tofauti kuelekea 2027. Bw Gachagua anajenga muungano imara wa upinzani huku akijaribu kuimarisha ushawishi wake Mlima Kenya.
Kwa upande wake, Rais Ruto anajaribu kujisawiri kama kiongozi aliye tayari kufanya kazi na yeyote anayekubali ajenda ya kitaifa, huku akimtenga Bw Gachagua kwa kucheza siasa za kikabila.
Rais pia amewataka wapinzani wake wawasilishe sera mbadala kwa Wakenya badala ya kutegemea matusi, kauli za chuki na uvamizi wa kisiasa.
Kauli yake inaashiria kuwa nafasi ya maridhiano ya kisiasa bado i wazi, lakini kwa masharti ushirikiano wowote hautatumika kukuza migawanyiko ya kikabila.
from Taifa Leo https://ift.tt/hzv9qrK
via IFTTT
Tags
TRENDING NEWS