Kaunti yapiga marufuku vijiko na uma hoteli za Mombasa kudumisha Uswahili

BUNGE la Kaunti ya Mombasa limepitisha sheria mpya inayopiga marufuku matumizi ya vyombo vya kulia chakula kama vijiko, uma na visu katika migahawa yote ndani ya Kisiwa cha Mombasa.

Hatua hiyo inalenga kukuza utamaduni wa Waswahili na kuimarisha eneo hilo kama kivutio cha utalii wa kitamaduni.

Sheria hiyo, iliyopitishwa Jumanne, inazitaka hoteli, migahawa na wauzaji wa vyakula ndani ya kisiwa hicho kuwahamasisha wateja kula kwa mikono, kulingana na mila za Pwani.

Madiwani waliounga mkono mswada huo walisema unalenga kulinda uhalisia wa utamaduni wa Kiswahili huku ukiwaruhusu wageni kupata uzoefu wa moja kwa moja.

“Kula kwa mikono ni sehemu muhimu ya utamaduni wetu na ni utambulisho tunaotaka kuuonyesha ulimwengu,” alisema mmoja wao.

Chini ya kanuni hizo mpya, biashara za vyakula zitalazimika kuweka vifaa vya kunawa mikono pamoja na kutoa mwongozo wa usafi kwa wateja.

Wale watakaoshindwa kutii wataadhibiwa kwa faini au hata kupokonywa leseni za biashara.

Maafisa wa kaunti walisema utekelezaji wa sheria hiyo utafanyika kwa awamu katika miezi ijayo ili kuwapa wafanyabiashara muda wa kujiandaa.

Wadau wa sekta ya utalii wamesifu hatua hiyo wakisema itaitofautisha Mombasa na maeneo mengine kwa kutoa uzoefu wa kipekee wa kitamaduni.

“Hatua hii inaifanya Mombasa isiwe tu eneo la fukwe bali kuwa kitovu hai cha utamaduni ambapo wageni wanaweza kujihusisha moja kwa moja na mila zetu,” alisema mwakilishi wa muungano wa sekta ya utalii.

Hata hivyo, baadhi ya wakazi na wamiliki wa biashara wameeleza wasiwasi kuhusu utekelezaji wake, hasa kwa migahawa inayotoa vyakula vya kimataifa.

Serikali ya kaunti imesema itashirikiana kwa karibu na wadau kushughulikia changamoto zitakazojitokeza wakati utekelezaji utakapoanza.



from Taifa Leo https://ift.tt/ijK9wCb
via IFTTT

Post a Comment

Previous Post Next Post